Ofisi ya Rais Sekretarieti ya Maadili ya viongozi wa Umma
Kanda ya Kasikazini imetoa mafunzo maalumu ya maadili kwa viongozi wa serikali
ya wanafunzi pamoja na CRs.
Katika mafunzo hayo yaliyotolewa Februari 7, 2026 viongozi
wameelimishwa mambo mbalimbali ya kimaadili ambayo yakifanywa yanaweza kuharibu
taswira na heshima ya chuo na kiongozi binafsi. Vile vile wameelimishwa namna
ya kujiepusha na mambo mbalimbali yasiyo ya kimaadili kama mgongano wa masilahi
katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.
Kutokana na kuongezeka kwa matumizi ya mitandao ya kijamii
kama facebook, Twitter (X), Instagram, Youtube na mingineyo, viongozi hao pia
wameelimishwa juu ya matumizi sahihi ya mitandao ya kijamii katika kujenga
wasifu wao (CV), kujitambulisha katika kile wanachofahamu kitaaluma na kuepuka
matumizi mabaya ya mitandao kama kueneza taarifa ambazo hazijathibitishwa.
Halikadharika, katika matumizi ya jina la taasisi (IAA),
viongozi hao pia wameonywa dhidi ya matumizi mabaya ya jina la taasisi kwani
hupelekea kuvunja heshima ambayo imejengwa kwa muda mrefu. Vile vile Ofisi ya
Rais Sekretarieti ya Maadili ya viongozi wa Umma Kanda ya Kasikazini imewaasa
viongozi kutumia vyema jina la taasisi katika maisha ya mtandaoni na jamii kwa
ujumla.
“Ambavyo wewe utajitambulisha huishii kusema John, wewe pia ni
mwanafunzi wa chuo maana yake unabeba dhamira mbili yaani dhamira ya kwako na
dhamira ya chuo” wamesema.
Wakizungumzia umuhimu wa kutoa elimu kwa wanafunzi wa vyuo Ofisi
ya Rais Sekretarieti ya Maadili ya viongozi wa Umma Kanda ya Kasikazini imesema
ni kuwaandaa kuja kuwa viongozi wazuri na wenye maadili thabiti.
“wewe ni kiongozi wa umma unayetarajiwa, kwaiyo kama Sekretarieti
ya Maadili ya viongozi wa Umma tunasimamia maadili ya viongozi, viongozi wa
sasa itafika hatua watastaafu nani atachukua hizo nafasi? Si ndio sisi wenyewe
tuliopo chuo? Ina maana tutakuja kuwajibika na maadili ya viongozi wa umma.” Wamesema.
Kwa upande wake Nadhiru Abdulnuru, Mkurugenzi wa huduma za
wanafunzi ameishukuru Ofisi ya Rais Sekretarieti ya Maadili ya viongozi wa Umma
Kanda ya Kasikazini kwa kuamua kutoa elimu ya maadili kwa viongozi wa serikali
ya wanafunzi IAA, kwani itasaidia kuwajenga na kuwawezesha kutekeleza majukumu
yao ya kila siku bila ukiukwaji wa sharia na maadili ya uongozi.
Naye, Rais wa Serikali ya wanafunzi-IAASO Francis Wambura
pia ameipongeza Sekretarieti ya Maadili ya viongozi wa Umma Kanda ya Kasikazini
kwa elimu hiyo, akisema mafunzo hayo ikiwezekana yatolewe kila mwezi kwa
viaongozi wa serikali ya wanafunzi na wanafunzi kwa ujumla, ili kuendelea
kuwajengea misingi imara ya uongozi wawapo chuoni na hata nje ya chuo.





